Kabla ya kuanza mchakato wa kujisajili, lazima uhakikishe kuwa mume/mke wako tayari amejiandikisha kivyake.
Zaidi ya mwaka mmoja baada ya Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA) kuchukua nafasi ya NHIF tarehe Oktoba 1, 2024, wakenya wengi bado wanahisi mfumo huu kuwa mgumu kuuelewa. Ikiwa unajaribu kuongeza mume/mke wako kama mtegemezi, mwongozo huu unakuonyesha hatua kwa hatua.
Kabla ya kuanza mchakato wa kujisajili, lazima uhakikishe kuwa mume/mke wako tayari amejiandikisha kivyake. Mfumo wa SHA utakataa jaribio lolote la kuongeza mtu ambaye hana wasifu wake kwenye SHA. Hili ndilo kosa la kawaida ambalo husababisha ucheleweshaji na usumbufu.
Hatua ya 1: Hakikisha mume/mke wako amejiandikisha
Mume/mke wako anaweza kujiandikisha kupitia njia zifuatazo:
- Mtandaoni: Tovuti ya SHA au Afya Yangu
- Simu ya mkononi: Piga *147#
- Ana kwa ana: Tembelea ofisi za SHA, Huduma Centre, au ofisi za TSC
Usajili huchukua dakika chache tu. Baada ya kukamilika, subiri saa 24 hadi 48 ili mfumo usasishwe kabla ya kumwongeza kama mtegemezi.
Hatua ya 2: Kusanya stakabadhi zinazohitajika
- Kabla ya kuanza, hakikisha una stakabadhi hizi:
- Kitambulisho cha Taifa (ID): Jina larimar lifanane na lililo kwenye maelezo ya SHA ya mume/mke wako
- Nambari ya simu iliyosajiliwa: Kwa uthibitisho kupitia OTP
- Uthibitisho wa ndoa: Cheti cha ndoa, hati ya kiapo, au barua kutoka kwa chifu
- Stakabadhi za ziada (ikiwa zinahitajika):
-Hati ya talaka (ikiwa unaondoa mume/mke wa awali)
-Cheti cha kifo (ikiwa ipo)
Chakuzingatia kwa watumishi wa umma: Malipo yako ya msingi yanahusisha mke mmoja. Ikiwa unataka kuongeza wake wengine, utalipa ada za ziada na utahitajika kusubiri kwa muda fulani.
Hatua ya 3: Ongeza mume/mke wako kupitia tovuti ya SHA
Fuata hatua hizi kwa makini:
- Ingia kwenye akaunti yako ya SHA
- Nenda kwenye Maelezo yako (My Profile)
- Chagua Wategemezi (Dependents)
- Bofya Ongeza Mtegemezi (Add Dependent)
Jaza taarifa zinazohitajika:
- Chagua “Mume/mke” (Spouse) kama aina ya uhusiano
- Ingiza nambari ya ID na jina kamili la mume/mke wako (kama lilivyo kwenye kitambulisho)
- Pakia stakabadhi zinazohitajika
5. Ingiza nambari ya simu ya mume/mke wako kwa uthibitisho
6. Ingiza msimbo wa OTP uliotumwa kwenye simu yake
7. Wasilisha ombi lako
Mchakato wa uthibitisho huchukua saa 24 hadi 48. Utapokea ujumbe baada ya mume/mke wako kuongezwa kwa mafanikio.
Hatua ya 4: Njia mbadala kupitia USSD
Ikiwa unapendelea kutumia simu ya rununu:
- Piga *147#
- Chagua Simamia Wategemezi (Manage Dependents)
- Chagua Ongeza Mtegemezi (Add Dependent)
- Ingiza nambari ya ID na nambari ya simu
- Kamilisha uthibitisho wa OTP
Unaweza kuwasilisha stakabadhi halisi baadaye katika kituo chochote cha huduma ya SHA ikiwa inahitajika.
Utatuzi wa changamoto: Tatizo la OTP
Kuchelewa kwa OTP ni moja ya malalamishi ya kawaida. Ripoti za hivi karibuni kutoka vituo vya afya nchini Kenya zinaonyesha kuwa changamoto za uthibitisho bado zinaathiri utoaji wa huduma. Ukikumbana na tatizo la OTP, jaribu yafuatayo:
- Subiri dakika chache kabla ya kuomba msimbo mpya
- Hakikisha umeingiza nambari sahihi ya simu
- Futa ujumbe ikiwa kisanduku chako cha ujumbe kimejaa
- Omba msimbo mpya kupitia mfumo
- Tembelea kituo cha huduma kwa usaidizi wa ana kwa ana
Dkt. Abdi Mohamed, Mwenyekiti wa SHA, alikiri changamoto hizi jijini Nairobi, akisema kuwa SHA bado iko katika kipindi cha mpito na inaendelea kuboresha mfumo, kuajiri wafanyakazi na kuimarisha miundombinu.
Hatua ya 5: Kusasisha au kuondoa Taarifa za mume/mke wako
Mabadiliko maishani yanahitaji kusasisha maelezo yako. Haya ndio unatakiwa kujua:
- Kubadilisha mume/mke kwanza: kuna muda wa kusubiri
- Mabadiliko ya ziada: muda wa kusubiri huwa mrefu Zaidi
- Kuondoa kutokana na kifo: unahitaji cheti cha kifo
- Kuondoa kutokana na talaka: hakuna muda wa kusubiri, lakini unahitaji hati ya talaka
Kumekuwa na ripoti za kutokulingana kwa taarifa katika akaunti za SHA. Baadhi ya watumiaji wameona wategemezi wasiowajua, huku wengine wakikosa kuona majina ya wategemezi wao halali.
Baada ya kufanya mabadiliko yoyote, hakikisha unakagua maelezo yako kwa makini kuthibitisha usahihi wa taarifa. Ukigundua makosa, yaripoti mara moja kupitia njia rasmi za usaidizi za SHA, kwani chaguo la kufuta taarifa binafsi bado halipo.
Licha ya kuwepo kwa changamoto kama ucheleweshaji wa OTP na matatizo ya kuingia kwenye mfumo, Dkt. Abdi Mohamed alisisitiza kuwa SHA inawasilisha zaidi ya mfumo mpya wa bima ya afya. Ni sehemu ya mageuzi makubwa ya ufadhili wa afya, ikijumuisha sheria ya Hazina ya Kuboresha vituo vya afya yaani FIF, inayolenga kuimarisha ufadhili wa hospitali na kuongeza uwajibikaji wa jamii.
Dkt Abdi aliongeza kuwa, kutokana na ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza nchini Kenya, nchi haiwezi kutegemea tu malipo ya mfukoni au misaada ya wafadhili wa nje. SHA inalenga kujenga mfumo endelevu wa ufadhili wa afya wa ndani.
Licha ya changamoto zinazoendelea, mfumo huu umefanikiwa kusajili takribani Wakenya milioni 29. Dkt. Abdi alitoa wito kwa umma kujadili kwa uelewa zaidi, wakizingatia muundo wa sera na uendelevu wa muda mrefu badala ya changamoto za muda mfupi za kiufundi.
Ikiwa utakumbana na matatizo yanayoendelea, tembelea ofisi ya SHA iliyo karibu nawe, Huduma Centre, au wasiliana na huduma kwa wateja wa SHA kupitia njia rasmi kwa usaidizi zaidi.




